Kilimo cha Bamia - Sehemu ya Tano (Growing Okra - Part Five)


SEHEMU YA TANO

Imehaririwa tarehe: 10/03/2021

B: MAGONJWA
1. Damping-off (Pythium spp., Rhizoctonia solani)
Ugonjwa huu huathiri mfumo wa ukuaji wa mmea, Viashiria vikubwa vya ugonjwa huu ni pamoja na uotaji hafifu wa mbegu na kufa kwa miche hali inayopelekea kuwa mazao dhaifu kwenye kitalu na shambani. Mbegu za bamia zinaweza kuoza zikiwa kwenye udongo. Miche michanga iliyoathiriwa huwa na muonekano wa majimaji na rangi ya kahawia kwenye shina usawa wa ardhi, pia sehemu hiyo ya shina usawa wa ardhi hudhoofu, hunyong'onyea na mwishowe mche hukatika usawa wa ardhi na kufa. Ugonjwa huu hupendelea sana udongo wenye jotoridi la chini na unyevu mwingi.

Picha: Miche michanga ya bamia iliyonyauka shambani baada ya kuoza usawa wa ardhi   Photo Credit: www.infonet-biovision.org

Picha: Mimea ya bamia iliyokomaa iliyoshambuliwa na ugonjwa huu   Photo Credit: www.ipmimages.org

Namna kuudhibiti
  • Tumia mbegu bora zisizo na magonjwa na zilizothibitishwa kitaalamu
  • Epuka kumwagilia maji mengi shambani na punguza matumizi makubwa ya mbolea za naitrojen (N) kama UREA n.k.
  • Badirisha mazao, Epuka kupanda bamia zako kwenye shamba ulilopanda bamia apo awali au zao lingine linalofanana au lililopo familia moja na bamia (Malvaceae) kama Pamba (Cotton) au usipande bamia maeneo yaliyopandwa Mibuyu (baobab trees) na Kokoa (cacao) kwani mibuyu na Kokoa ni familia moja na Bamia (Malvaceae).
2. Early Blight (Alternaria sokani)
Huu ni ugonjwa wa ukungu wa kwenye majani unaosababishwa na fangasi. Majani huwa na madoa madoa ya mviringo yenye ukubwa hadi kufikia mm 12, madoa hayo huwa na rangi ya kahawia.

Picha: Ugonjwa wa early bright kwenye majani    Photo Credit: www.infonet-biovision.org

Namna ya kuudhibiti
  • Panda mbegu ya bamia zinazovumilia ugonjwa huu kama "Rio Grade".
  • Tumia mbegu bora zisizo na magonjwa na zilizothibitishwa kitaalamu. Kama unatumia mbegu zako ulizozalisha mwenyewe hakikisha unazitibu kwa kutumia maji ya moto. Namna ya kuzitibu mbegu kwa kutumia maji ya moto nitaeleza vizuri kwenye makala zijazo, hatua kwa hatua.
  • Usipande bamia au mazao mengine yanayopata ugonjwa huu kama nyanya n.k kwenye eneo lilelile mfululizo. Badilisha mazao kwa kupanda mazao mengine jamii ya Nafaka,mikunde n.k.
  • Kama ugonjwa umeenea sana tumia dawa ya ukungu kama Blue Copper (Copper Hydroxide) na dawa nyinginezo.
3. Fusarium wilt (Fusarium oxysporum f.sp.vasinfectum)
Huu ni Ugonjwa wa ukungu, husababishwa na kimelea cha Fangasi kinachoitwa Fusarium. Ni ugonjwa ambao vimelea huanzia kwenye mbegu na kwenye Udongo (Seed and Soil-borne)

Picha: Shamba la bamia lililoathiriwa na Mnyauko fuzari (Fuzarium Wilt)  Photo Credit: www.researchgate.net

Dalili za Ugonjwa
  • Mmea ulioathirika hudumaa
  • Majani hubadilika rangi na kuwa njano, hunyauka na baadae hupukutika
  • Mara nyingi majani ya chini huathirika sana
  • Ukikata shina la Mmea ulioathirika katikati (crosswise), utaona rangi ya kahawia.
  • Mmea hunyauka wote, Hali ifuatayo huongeza kasi ya ugonjwa; Uhaba wa maji, udongo wenye joto la uvuguvugu (warm soil temperature), Udongo wenye Tindikali (Acidic soils) na kiwango kikubwa cha kirutubisho cha Nitrojeni kwenye udongo. Vilevile minyoo wa kwenye udongo (Root nematodes) wakivamia mizizi ya mmea huongeza kasi ya ugonjwa huu.
Namna ya kuudhibiti
  • Tumia mbegu bora zisizo na magonjwa na zilizothibitishwa kitaalamu.
  • Kama una mbegu ulizozitengeneza mwenyewe, hakikisha unazitibu mbegu hizo kwa kutumia dawa za kuua vimelea vya fangasi (biopesticide) kama Trichoderma viride na nyinginezo.
  • Dhibiti minyoo wa kwenye udongo (Root-knot nematodes). Namna ya kudhibiti minyoo hawa nimeeleza vizuri kwenye makala za nyuma, Rejea makala za nyuma utapata  maelezo mazuri kuhusiana na mnyoo huyu.
  • Dhibiti magugu shambani, hii itasaidia kupunguza kasi ya ugonjwa na kupunguza idadi ya minyoo hao kwenye udongo.
4. Powdery mildew (Leveillula taurica / Oidiopsis taurica)
Ugonjwa huu husababishwa na kimelea cha fangasi, vimelea vya ugonjwa huvamia Majani, Mashina, maua na matunda. Pia ugonjwa huu huenea zaidi kukiwa na unyevu hewa (Humidity) mwingi kuanzia 52 hadi 75% na joto ridi kuanzia 26 hadi 27°C.

 Picha: Ugonjwa huu kama unavyoonekana kwenye majani     Photo Credit: www.apsnet.org

 Picha: Ugonjwa huu kama unavyoonekana kwenye majani     Photo Credit: www.flickr.com


 Picha: Ugonjwa huu kama unavyoonekana kwenye majani    Photo Credit: www.flickr.com

Dalili za Ugonjwa
  • Kunakua na Ungaunga mweupe (white coating resembling a fine talcum powder) uliotengeneza tabaka jeupe na ulioshikamana juu ya majani ya chini na ya juu. Tabaka hilo jeupe la unga ndio ukuaji wa fangasi.
  • Ugonjwa ukizidi husababisha majani yaliyoathirika kujikunja kwa juu na hatimae huwa kama yameungua.
  • Vilevile ugonjwa huu huvamia mashina, vishikizi vya maua na matunda ya bamia.
Namna ya kudhibiti
  • Hakikisha shamba lako linakua safi wakati wote kwa kuondoa magugu ndani ya shamba na pembeni ya shamba.
  • Usipande bamia kwenye shamba lililopandwa mazao yanayoelekeana na bamia kama Pamba.
  • Tumia dawa mbalimbali za ukungu zenye salfa (sulphur)
5. Bacterial blight ( Xanthomonas campestris p.v. malvacearum)
Ni ugonjwa unaosababishwa na bakteria anaeitwa Xanthomonas campestris, bakteria hawa husambazwa kupitia mbegu na michapo ya matone ya maji (water splash).

Picha: Ugonjwa huu kama unavyoonekana kwenye majani  Photo Credit: www.infonet-biovision.org


Picha: Ugonjwa huu kama unavyoonekana kwenye tunda changa la bamia  Photo Credit: www.infonet-biovision.org

Dalili za ugonjwa
  • Madoa madoa huonekana  kwenye majani na matunda.
  • Madoa ya kwenye majani huwa na majimaji na huonekana sana chini ya jani.
  • Madoa ya kwenye matunda huwa na majimaji (water-soaked) na ya mviringo, baadae madoa hayo huungana kutengeneza rangi nyeusi yenye muonekano wa mafutamafuta. Madoa yote huonekana yana unato (waxy) na yanang'aa.
Namna ya kudhibiti
  • Tumia mbegu zilizothibitishwa kitaalamu na zisizo na magonjwa
  • Epuka umwagiliaji wa juu ya mmea (Overhead irrigation).
  • Epuka kufanya kazi shambani wakati kuna ubichi.
  • Ondoa mabaki ya mimea shambani baada ya kuvuna.
  • Pulizia dawa za ukungu zenye kiuasumu cha Kopa (Copper).
6. Black mould (Cercospora abelmoschi)
Hawa ni fangasi weusi ambao huota na kuongezeka sana maeneo yenye unyevu na joto la uvuguvugu. Huota kama masizi au oili chafu.

 Picha: Ugonjwa huu kama unavyoonekana kwenye majani    Photo Credit: www. m-crop.blogspot.com

 Picha: Ugonjwa huu kama unavyoonekana kwenye majani    Photo Credit: www.infonet-biovision.org

Dalili za ugonjwa
  • Madoa meusi yenye maumbile tofauti tofauti huonekana kwenye majani.
  • Kuota kwa fangasi zinazofanana na masizi chini ya jani, lakini kama hali ya ugonjwa imekua mbaya sana na kuna unyevu-hewa (humidity) mwingi basi fangasi hao kama masizi huonekana juu ya jani.
  • Magonjwa yaliyoathiriwa sana na ugonjwa huu hujikunja, hukauka na hatimae hudondoka.
Namna ya kudhibiti
  • Panda bamia kwa nafasi inayotakiwa kitaalamu, epuka kuyafanya mashina ya bamia kugusana na mashina mengine ya bamia.
  • Badilisha mazao kwa kupanda mazao yasiyofanana na bamia kama Mahindi n.k.
  • Epuka umwagiliaji wa juu ya mmea (Overhead Irrigation).
  • Tumia dawa za ukungu zenye kiua sumu cha Kopa (Copper).
7. Choanephora Flower and Fruit Rot (Kuoza maua na matunda)
Ugonjwa huu husababishwa na fangasi aina ya Choanephora cucurbitarum, ni ugonjwa unaoyakumba mazao mengi ya mboga mboga ikiwemo maharage, bilinganya, cantaloupe, bamia, mbaazi, maboga n.k. Jina jingine la ugonjwa huu hujulikana kwa lugha ya kimombo kama Wet rot au Blossom end rot, ingawaje pia ugonjwa huu huweweza kufananishwa na magonjwa mengine ya fangasi kama Botrytis gray mold na Rhizopus au Mucor rots.

Ugonjwa huu huongezwa kasi na kipindi kirefu cha joto kuanzia nyuzi joto 25ºC hadi 27ºC na kiasi kikubwa cha unyevu wa udongo shambani, Vimelea vya fangasi (Choanephora cucurbitarum) huvamia maua na matunda madogo yanayokua. Matunda yaliyo karibu na ardhi au yaliyopo juu ya ardhi hua hatarini zaidi kuathirika na ugonjwa huu. Tazama picha zifuatazo kuhusiana na ugonjwa huu;





Dalili za ugonjwa
  • Tunda huoza kuanzia mwishoni (sehemu iliyochongoka), sehemu hiyo huwa laini na yenye majimaji, pia fangasi kama nyuzinyuzi laini huota kwenye sehemu iliyooza na kwenye maua. Nyuzinyuzi laini wa fangasi hao huwa na rangi nyeupe iliyochangamana na kijivu pamoja na madoa madoa madogo meusi.
Namna ya kudhibiti
  • Panda bamia zako eneo lisilotwamisha maji, kama eneo lina maji mengi tengeneza matuta ili kupunguza maji, juu ya matuta hayo utapanda bamia. Pia kama umeshapanda bamia kwenye eneo hilo na umeona athari za ugonjwa huu punguza maji shambani kwa kutengeneza mifereji inayotoa maji kwenda nje ya shamba, vilevile unaweza kuzuia maji yasiingie shambani kwa kutengeneza matuta ya kuzuia maji na kuyachepusha eneo jingine.
  • Panda bamia zako kwa nafasi kama inavyoshauliwa kitaalamu, nafasi hiyo inasaidia kuruhusu hewa kupenya shambani na kupunguza unyevu wa udongo.
  • Hakikisha shamba lako ni safi wakati wote kwa kuondoa magugu mara tu yanapoota, hali hii itasaidia kuruhusu hewa kupenya na kupunguza unyevu wa udongo.
  • Tumia matandazo ya nyasi au ya plastiki (plastic mulch) kwenye eneo la kuzunguka shina ili kuzuia matunda yasiguse ardhi.
  • Kwa kipindi cha kiangazi epuka umwagiliaji wa juu (overhead irrigation), hii itapunguza unyevu uliokithiri kwenye majani ambao baadae huongeza athari ya ugonjwa. Badala yake tumia umwagiliaji wa mifereji (surface irrigation).
  • Matumizi ya dawa za kuua fangasi hawa (Dawa za ukungu) huwa hazina ufanisi kwa sababu kipindindi hicho maua na matua hukua kwa kasi sana, kwa hiyo hiyo tumia njia kama nilivyozieleza hapo juu.
  • Njia nyingine ya kudhibiti ni kubadirisha mazao kwa kupanda mazao mengine tofauti na mazao ya mbogamboga, kwa sababu vimelea hivi hukaa kwenye udongo au masalia ya mimea ya bamia kwa msimu mzima wakisubili mazingira wezeshi kama unyevu na joto. Mazingira wezeshi yakipatikana mbegu (spores) za vimelea hivyo husambazwa kwa upepo, mchapo wa maji (splashing water), nyuki, cucumber beetles na wadudu wengine.
MAVUNO
Aina nyingi za bamia huwa tayari kuvunwa ikifikia siku 45 hadi 60 baada ya kupanda. Matunda ya bamia yanatakiwa yavunwe yakiwa laini na yasiyokomaa sana na yaliyofikia urefu wa sm 6 - 15. Kadiri unavyochuma matunda yaliyokomaa ndivyo jinsi matunda mengine mapya yanavyozaliwa, Kwa hali ya hewa ya maeneo mengi hapa nchini Tanzania  mkulima ataendelea kuchuma bamia zake kwa siku 45 zaidi baada ya kuchuma mchumo wa kwanza. Kwa kawaida inatakiwa mkulima achume bamia zake kila baada ya siku 1 au 2 kupita, ili kupata bamia zenye ukubwa na ubora unahitajika sokoni. Kwa ujumla matunda ya bamia yanatakiwa yachumwe siku 4 hadi 6 baada ya mmea  kutoa maua. Shamba la bamia lililotunzwa vizuri huzalisha Tani 7 (Kilo 7000) kwa ekari 1.

NB:
Haitakiwi kuvuna bamia wakati mvua inanyesha au wakati kuna unyevu mwingi. Unyevu unapokuwa mwingi shambani husababisha matunda ya bamia yaliyovunwa kupata ukungu au Fangasi, matunda yenye Fangasi huoza haraka sana. Kwa hiyo inatakiwa matunda ya bamia yavunwe wakati ambao hakuna mvua na hakuna unyevu mwingi shambani, Pia ni vizuri zaidi yakavunwa siku ile ile ya kupelekwa sokoni.

Uhifadhi wa matunda ya bamia baada ya mavuno
Matunda ya bamia huharibika haraka sana kama yasipohifadhiwa vema. Epuka kuchubua ngozi ya bamia, kwa sababu michubuko hiyo hupelekea bamia kupoteza maji na kunyauka na kupoteza ubora wake.


*MWISHO WA MAKALA HII*

Makala na: Lusubilo A. Mwaijengo

1 Comments

Post a Comment

Previous Post Next Post