Kilimo bora cha Mihogo - Sehemu ya Kwanza (Growing Cassava - Part One)


SEHEMU YA KWANZA

Zao la Muhogo (Cassava) hulimwa sana nchini Tanzania, afrika mashariki, Afrika na Duniani kwa ujumla hususani kwa maeneo ya pwani ya Bahari au Maziwa mbalimbali.

Zao hili ni muhimu sana kwa matumizi ya chakula pia humfaa mkulima mdogo mdogo kwa sababu huitaji utaalamu kidogo wa uzalishaji pamoja pembejeo kidogo.

Pia zao hili huvumilia ukame, linaweza kutoa mavuno yanayorizisha hata kama kukiwa na ukame sana. Pia umuhimu wake mwingine ni kwamba, mihogo inaweza kukaa kwenye udongo miezi kadhaa bila kuharibika, hivyo inaweza kutumika kama akiba ya chakula wakati wa njaa.


MAZINGIRA
Zao la muhogo hupendelea maeneo yenye hali ya joto, ndio maana maeneo ya pwani ya bahari au maziwa hufaa sana kwa zao hili. Zao hili hustawi vema kwenye muinuko wa ardhi kuanzia mita 0 hadi 1500 kutoka usawa wa bahari.

Hali ya joto linalohitajika kwa zao hili ni nyuzi joto 20°C hadi 30°C. Zao hili hufanya vizuri kwenye maeneo yenye mvua kiasi cha mm 500 hadi 6000 kwa mwaka. Kiwango mahsusi cha mvua kinachohitajika ni mm 1000 hadi 1500 kwa mwaka ila pasiwepo na ukame sana kwa wakati huo.

Zao la muhogo hupendelea udongo tifutifu wenye kichanga (Sandy loams). Zao hili huweza kutoa mavuno hata kwenye udongo ulioathiriwa na mmomonyoko wa udongo ambapo mazao mengine hayakukubali. Hivyo udongo wenye changalawe au kokoto haufai kwa zao hili, pia udongo usiopitisha na unaotwamisha maji kama mfinyanzi nao haufai.

Pia zao hili hupendelea udongo wenye tindikali kiasi cha pH 5.5 hadi 7.5, kiwango kikishuka chini ya pH 5.5 huo udongo haufai kwani kunakua na Asidi nyingi. Pia kiwango kikiongezeka zaidi ya pH 7.5 huo udongo haufai kwani kunakua na bezi nyingi (Alkaline). Kiwango cha tindikali kikipungua au kikiongezeka zaidi ya pH 5.5 - 7.5, basi zao la muhogo hudumaa na kupunguza uzalishaji. Vilevile zao la muhogo halifai kwenye udongo wenye Rutuba sana kwani litatoa majani mengi kuliko matunda ya muhogo.


AINA
Kuna aina mbalimbali za muhogo zinazopandwa nchini Tanzania. Wakulima wengi hupanda mbegu za kienyeji, siku zijazo nitakuletea mbegu bora za muhogo zilizofanyiwa utafiti nchini Tanzania.


KUANDAA SHAMBA
Kabla ya kuandaa shamba hakikisha eneo lako linakidhi vigezo vya kilimo hiki kama ifuatavyo;
  1. Eneo la kupanda muhogo liwe sehemu tambalale au lenye mteremko kiasi (Gently sloping land). Maeneo yenye mtelemko mkali (Steep slopes) hayafai kwa sababu ni rahisi kutokea mmomonyoko wa udongo.
  2. Maeneo ya mabonde hayafai kwa kilimo hiki kwani maeneo haya hutunza maji hivyo hali ya kuwepo kwa maji husababisha mizizi ya mihogo kutokukua vema.
  3. Pia ni vyema kupata historia ya shamba kama; aina ya mazao yaliyopandwa msimu uliopita, magonjwa na wadudu waliokuwepo n.k. Hii ina maana kwamba shamba lilopandwa muhogo kwa misimu kadhaa mfululizo halifai kupanda tena muhogo kwa sababu magonjwa na wadudu walewale wa muhogo wataendelea kuongezeka. Badirisha mazao, ingawaje zao la muhogo linaweza kupandwa kwa misimu kadhaa mfululizo kwenye eneo moja pasipo kupunguza uzalishaji, tofauti na mazao mengine. Ili kuongeza uzalishaji inampasa mkulima kubadilisha mazao kwa kupanda mazao mengine tofauti na muhogo au mazao mengine jamii ya mizizi kama; maharage, kunde, mazao ya nafaka n.k
Baada ya kupata eneo zuri linalofaa, lima vizuri shamba lako kwa kina cha kutosha. Zao la muhogo hupandwa kwa kawaida au kwenye matuta. Kupanda kwenye matuta kunafaa sana kwenye maeneo yenye mvua nyingi kuanzia mm 1200 na kuendelea kwa mwaka.

Kupanda kwa matuta hakutoi mavuno mengi tofauti na kupanda kawaida, ingawaje kupanda kwa matuta husaidia sana kwa maeneo yenye miteremko ili kuzuia mmomonyoko wa udongo.


KUPANDA
Zao la muhogo hupandwa kwa kutumia mashina ya mmea wa muhogo uliokomaa kwa kukata vipande vipande vyenye urefu wa sm 20 - 30 na kipenyo cha mm 20 - 25. Panda vipande vyako mwanzoni mwa mvua za kwanza.

A: Kuandaa vipande vya mashina
Vipande hivyo vya kupanda lazima viwe na macho au mafundo 5 hadi 8, pia vipande hivyo lazima vitoke kwenye mmea wa muhogo wenye afya na wenye umri wa miezi 8 hadi 14.

Picha: Kuandaa vipande vya kupandia

Vipande hivyo inatakiwa viwe vimekomaa na vimetoka sehemu ya katikati ya shina, sehemu iliyokomaa hutoa mavuno mengi kuliko sehemu yenye mashina machanga. Vilevile mashina malefu ya kupandia hutoa mavuno mengi kuliko mashina mafupi.

Vitibu vipande hivyo vya mashina kwa maji ya vugu vugu, ili kuua na kutibu magonjwa mbalimbali yaliyopo kwenye mashina. Kinachofanyika vipande hivi vya mashina hudumbukizwa kwenye maji ya vugu vugu kwa dakika 5 hadi 10. Namna ya kuandaa maji hayo ya vugu vugu; Changanya maji ya moto yaliyochemka na maji ya baridi kwa uwiano wa 1:1, yaani kama umechemsha maji ya moto kiasi cha ndoo moja ya lita 10 basi uchanganye na maji ya baridi kiasi kicho hicho cha lita 10.

Inatakiwa vipande hivyo vya mashina vipandwe haraka iwezekanavyo mara tu baada ya kuandaliwa, ili kuepusha kuharibika kabla ya kupandwa.

Photo Credit: IITA genebank          Website: www.cropgenebank.sgrp.cgiar.org

B: Kupanda
Mihogo hupandwa kwa nafasi ya mita 1 shina hadi shina na mita 1 mstari hadi mstari (mita 1 x mita 1), ina maana kutakua na vipande 10000 kwa hekta 1 au vipande 4000 kwa ekari moja.

Vipande vya mashina ya muhogo hupandwa kwa wima au kwa kuchegama (at an angle), wakati wa kupanda hakikisha macho ya vipande hivyo (buds) yameangalia juu. Ina maana usigeuze vipande hivyo kuwa juu - chini kwani kutakua na uzalishaji mdogo wa mihogo.

Upandaji wa wima au kuchegama hutegemea aina ya udongo na hali ya unyevu wa udongo, kwa mfano ukipanda vipande vyako wakati wa kiangazi au masika inatakiwa uvichomeke ardhini kwa kuchegama (at an angle) na sehemu kubwa ya macho iwe ardhini na ufukie udongo vizuri. Kama ni udongo wa kichanga inatakiwa vipande hivyo vipandwe wima, hii itasaidia mmea kuwa na mizizi mirefu.

Picha: Vipande vya muhogo vilivyopandwa Wima (kushoto) na Kuchegama (Kulia)

NB:
Haitakiwi upande vipande vyako kwa ulalo (Horizontal), kwa sababu kutazaliwa mashina mengi na mizizi itakua juu juu, hali itakayopelekea urahisi wa kuharibiwa na panya au ndege.


Makala na: Lusubilo A. Mwaijengo

Post a Comment

Previous Post Next Post