Kilimo Bora cha Pilipili kichaa - Sehemu ya Tisa (Growing Chili pepper - Part Nine)


KILIMO CHA PILIPILI KICHAA SEHEMU YA TISA

B: MAGONJWA

1. Fusarium wilt (Mnyauko Fuzari)
Huu ni ugonjwa wa kuvu unaosababishwa na vimelea vya fangasi, vimelea hawa husambazwa kupitia udongo (soil borne fungal disease), huenea sana wakati wakati wa joto kali. Ugonjwa huu huathiri mmea wote ikiwemo mizizi, mashina, matawi na majani.

Picha: Fusarium wilt   shared under a Creative commons license

Athari
- Mmea ulioathirika huwa dhaifu na majani yake huwa ya njano.
- Ukikata shina usawa wa ardhi utaona rangi ya kahawia iliyochangamana na nyekundu, pia ukipasua kwa ndani zaidi utaona rangi ya kutu.

Namna ya kudhibiti
- Hakikisha usafi wa shamba
- Badilisha mazao
- Kama udongo unatwamisha maji, tengeneza vimfereji vya kuondosha maji (drainage channels)
- Kama umetumia vyombo maalumu kwa kuotesha miche, hakikisha unaviosha vizuri na kuvitunza mahala pasafi.
- Lima shamba lako kwa kina cha kutosha na kuliacha shamba hilo lipigwe na jua kwa miezi kadhaa kabla ya kupanda. Hii itasaidia kuua vimelea wanaosababisha ugonjwa huu.
- Mimea iliyoathirika iondolewe shambani pamoja na udongo uliopo kwenye mizizi na ichomwe moto.
- Weka matandazo ya nyasi kavu (mulching), matandazo haya husaidia kudhibiti joto la udongo. Ugonjwa huu huenea sana wakati joto kali.

2. Southern blight (Sclerotium wilt)
Ugonjwa huu husababishwa na vimelea wa fangasi (Kuvu), ugonjwa huu hutokea kwa muda mfupi hususani kwa maeneo yenye joto jingi na unyevu mwingi.

    Picha: Southern blight   Photo Credit: www.seminis-us.com

Athari
- Majani ya chini hunyauka
- Fangasi zenye rangi nyeupe huota kwenye mashina

Namna ya kudhibiti
- Mimea yote iliyoathirika ing'olewe pamoja na udongo wake kwenye mizizi kisha ipelekwe mbali na eneo la shamba na ichomwe moto.
- Lima shamba lako kwa kina cha kutosha hii itasaidia kuwaweka fangasi hao chini ya ukanda wa mizizi (Below the root zone).

3. Anthracnose
Ugonjwa huu huathiri sana zao la pilipili, husababishwa na vimelea wa fangasi (Kuvu). Husambazwa kutoka mmea mmoja hadi mwingine au kutoka msimu mmoja hadi mwingine kupitia masalia ya mimea yenye ugonjwa huu.

Picha: Anthracnose   Photo Credit: www.ipmimages.org

Picha: Anthracnose    Photo Credit: www.pestnet.org

Athari
- Matunda ya pilipili huwa na maeneo meusi yaliyobonyea na yenye majimaji baadae maeneo haya hubadirika na kutengeneza utando mweusi. Pia unato wenye rangi ya pinki huweza kuonekana kwenye matunda, unato huu ni mbegu (spores) ambazo husambaza ugonjwa huu wa fangasi.
- Matunda yaliyoathirika huoza.

Namna ya kudhibiti
- Ondoa na choma moto mimea yote iliyoathirika shambani pia baada ya kuvuna choma moto masalia yote, kwa sababu ugonjwa huu huenezwa kupitia masalia ya mimea iliyoathirika.
- Badirisha mazao
- Tumia mbegu zilizothibitishwa kitaalamu kwa sababu ugonjwa huu husambazwa kupitia mbegu zilizotoka kwenye mmea ulioathirika na ugonjwa huu (seed-borne).
- Kama unataka kuaandaa mbegu kutoka kwenye mimea uliyopanda, hakikisha unachagua mimea yenye afya na isiyokua na ugonjwa.
- Vuna matunda ya pilipili mara tu yanapokomaa, kufanya hivi husaidia kupunguza ya ugonjwa huu kujijenga kwenye matunda.

4. Bacterial spot (Madoa bakteria)
Ugonjwa huu husababiswa na vimelea wa bakteria, husambaa haraka kwenye maeneo yenye joto jingi na unyevu mwingi. Vilevile ugonjwa huu husambazwa kupitia mbegu (seed-borne).

Penn State Department of Plant Pathology & Environmental Microbiology Archives , Penn State University, Bugwood.org
Creative Commons License   licensed under a Creative Commons Attribution-Noncommercial 3.0 License

Athari
- Husababisha madoa madoa yenye rangi ya kahawia chini ya majani (Bacterial spots) na kwenye matunda.
- Bakteria hawa huingia kwenye matunda na kusababisha matunda kuoza.

Namna ya kudhibiti
- Usiandae mbegu za kupanda kutoka kwenye mmea ulioathorika na ugonjwa huu.
- Tumia dawa mbalimbali za ukungu hususani zenye kiua sumu cha mancozeb.

5. Magonjwa ya virusi (Viruses disease)
Kuna magonjwa mengi ya virusi yanayoathiri zao la pilipili, magonjwa hayo makubwa ni pamoja na Tobacco Etch Virus (TEV) na Potato Virus Y (PVY). Magonjwa mengine ni pamoja na Pepper Mottle Virus (PeMV), Pepper Veinal Mottle Virus (PVMV), Tobacco Mosaic Virus (TMV) na Cucumber Mosaic Virus (CMV). Magonjwa yote hufanana dalili na athari kwenye mmea.

Florida Division of Plant Industry , Florida Department of Agriculture and Consumer Services, Bugwood.org
Creative Commons License   licensed under a Creative Commons Attribution-Noncommercial 3.0 License.

Athari
- Majani hubadilika rangi na kuwa ya njano na hujikunja kuelekea juu.
- Mmea ulioathirika hudumaa na hutoa matunda kidogo.

Namna ya kudhibiti
Njia madhubuti ya kudhibiti ugonjwa huu ni kukinga mmea usipate maambukizi ya virusi hivi. Zifuatazo ni njia mahsusi za kudhibiti ugonjwa huu.

- Tumia mbegu zilizothibitishwa kitaalamu kwani ugonjwa kama TMV husambazwa kupitia mbegu.
- Hakikisha mmea hauna wadudu waharibifu wanaosambaza ugonjwa huu kama Vidukari mafuta (Aphids) na wadudu wengine. Pulizia dawa mbalimbali kuwaondoa wadudu hawa.
- Pia unaweza ukapanda mazao kama mahindi kuzunguka mipaka ya shamba lako (berrier crops), zao la mahindi huzuia wadudu kama Vidukari mafuta (Aphids) kuingia shambani. Pia punguza kushika mimea pasipo sababu, kwani unaweza kusambaza ugonjwa kwenye mimea yenye afya.
- Badirisha mazao na kuondoa magugu kama Black nightshade, magugu haya huvutia wadudu wanaosambaza magonjwa haya ya virusi. Tazama picha ya gugu hili kulifahamu.

Picha: Black night shade 

MAVUNO
Pilipili kichaa huwa tayari kuvunwa baada ya wiki 8 hadi 12 baada ya kupandikizwa au wiki 3 hadi 6 baada ya kutoa maua, ingawaje hii itategemeana na aina ya mbegu na hali ya hewa pamoja au msimu husika.

Matunda yakikomaa hubadirika rangi kutoka kijani kuwa njano, rangi ya chungwa au nyekundu. Kwa hiyo uhitaji wa soko wa rangi mahsusi ya pilipili utampa wasaa mkulima avune pilipili hizo wakati gani aidha wakati ziko mbichi au wakati zimeiva, vuna pilipili zako mara moja kwa wiki.

Kama utatunza shamba lako vizuri na kufwata mbinu za kilimo bora kama nilivyoeleza kwenye makala hii, utaweza kuvuna kilo 1000 hadi 3000 kwa ekari moja (tani 1 hadi 3 kwa ekari moja) sawa na gramu 600 za pilipili mbichi kwa mche mmoja wa pilipili.


MWISHO WA MAKALA HII

Makala na: Lusubilo A. Mwaijengo

2 Comments

  1. Asante kwa elimu, iwapo kuna kitabu naomba kujua namna ya kukipata

    ReplyDelete
  2. Asante kwa somo hili la Pilipili, somo linaeleweka vizuri.

    ReplyDelete

Post a Comment

Previous Post Next Post