Kilimo Bora cha Pilipili kichaa - Sehemu ya Sita (Growing Chili pepper - Part Six)


KILIMO CHA PILIPILI KICHAA SEHEMU YA SITA

KUPIMA UDONGO
Hatua hii ni muhimu sana kwa mazao yote ikiwemo zao la pilipili, kupima udongo kutasaidia kufahamu hali ya udongo kama virutubisho vilivyomo pamoja hali ya tindikali ya udongo (pH). Zao la pilipili hufanya vizuri kwenye udongo usiotwamisha maji na wenye kiasi cha tindikali (pH) kuanzia 5.5 - 7.5 na kiasi kidogo cha kirutubisho cha Naitrojeni, kwa hiyo pH ikipungua au ikizidi zaidi ya kiwango hicho mmea hautafanya vizuri. Ukitaka kupima udongo wa shamba lako waone wataalamu wa kilimo (Ma Afisa Kilimo) walio karibu nawe.

Kwa mfano kama ikitokea shamba lako lina pH kuanzia 3.9 - 5.0, shamba lako lina kiwango kikubwa cha asidi (acids), hali hii inahitaji kuiongeza hiyo pH hadi kufikia 7.0.

Hali hiyo inabadilishwa kwa kutumia chokaa (Lime), kama ikitokea shamba lako lina pH 4.0, hivyo kitahitajika kiasi cha Tani 3.6 (3.6 Tonnes) za chokaa kuongeza pH hadi 7.0 kwa ekari moja.

Chokaa huongezwa wakati wa kuandaa shamba kabla ya kupanda, chokaa hii huchanganywa vizuri kwenye udongo.

Kama udongo umepimwa na kuna upungufu wa virutubisho aidha Nitrogen, Phosphorus, Potassium, Magnesium, sulfur, Zinc au Calcium n.k., mtaalamu wa kilimo atakushauli utumie kiasi gani cha mbolea kwenye udongo huo.

KUANDAA SHAMBA
Kama yalivyo mazao mengine, shamba lililokusudiwa kupanda pilipili lazima lilimwe vizuri, ikiambatana na maandalizi ya kitalu kwa ajili ya kusia mbegu za pilipili. Vilevile kama shamba lako limegundulika lina kiwango kikubwa cha asidi (acids) mfano pH 4.0, basi ukishalima vizuri, ni wakati wa kuchanganya udongo wako na chokaa (Lime) kiasi cha Tani 3.6 kwa ekari moja. Kama itagundulika pH ya udongo wako ni kuanzia 5.5 - 7.5 basi shamba lako linafaa kupanda zao hili.

KUANDAA KITALU
Mbegu za pilipili/pilipili kichaa hupandwa kwanza kwenye kitalu ndipo baadae huamishiwa shambani. Yafwatayo ni maelezo ya kina namna ya kuandaa kitalu;

1. Lima vizuri eneo lako la kutengenezea kitalu

2. Tengeneza matuta yenye upana wa mita moja na urefu wowote.

3. Weka mbolea ya samadi iliyooza vizuri, kiasi cha ndoo moja kubwa ya samadi kwa m² moja, mfano kama tuta lako lina urefu wa mita 5, ina maana eneo lake ni m² 5, sawa na ndoo kubwa 5 za samadi. Ichanganye vizuri mbolea hiyo na udongo, kisha sawazisha juu ya tuta pawe tambalale.

Hakikisha mbolea ya samadi unayotumia imeoza vizuri, kwani mbolea ya samadi mbichi huongeza uwezekano wa minyoo fundo (Root nematodes) kwenye mizizi ya pilipili.

4. Baada ya kusawazisha matuta yako, tandaza juu ya tuta nyasi kavu zilizokauka vizuri, kisha choma moto nyasi hizo zikiwa juu ya tuta mpaka ziungue zote. Moto wa nyasi hizi husaidia kuua wadudu na magonjwa ya kwenye udongo ambayo baadae huweza kuathiri mche wa pilipili.

5. Baada ya nyasi kuungua acha tuta lako lipoe kabla ya kusia mbegu.

6. Baada ya tuta kupoa, tengeneza vimfereji kukatisha tuta vinavyoachana kwa sm 10.

7. Sia mbegu kwa kuziachilia kidogo kidogo kwenye vimfereji hivyo, kisha fukia na udongo kiasi.

8. Baada ya kufukia vizuri, tandaza nyasi kiasi kavu na laini juu ya tuta, kisha mwagilia maji vizuri. Nyasi hizi husaidia kuzuia mbegu zilizopandwa kutawanyika wakati wa kumwagilia. Nyasi hizo huondolewa baada ya wiki moja tangu kusia mbegu, wakati huu mbegu zote huwa zinakua zimeota.

9. Baada ya kumwagilia maji, pulizia dawa ya kuvu (ukungu) na wadudu ju ya nyasi hizo. Hii itasaidia mbegu zote kuota na kuepusha kupata ugonjwa wa kuoza shina usawa wa ardhi (dumping off).

10. Baada ya wiki moja tangu kusia mbegu, ondoa taratibu nyasi hizo, kisha tengeneza kichanja chenye kimo cha mita 1 juu ta tuta, alafu juu tandaza nyasi kavu kwa ajili ya kivuli. Kichanja hiki husaidia kuepusha miche dhidi ya jua kali au mvua kubwa. Endelea kumwagilia maji asubuhi na jioni kila siku.

NB:
Utaratibu huu wa kuandaa kitalu ni kwa mazao yote yanayohitaji kuandaa kitalu ikiwemo zao la pilipili.

KUPANDIKIZA MICHE SHAMBANI
Miche huwa tayari kupandikizwa shambani baada ya siku 30 - 40, wakati yakiwa na majani 8 - 10. Wiki moja kabla ya kupandikiza (siku 23 - 33) ondoa kichanja na punguza kiwango cha kumwagilia maji. Kama ulikua unamwagilia asubuhi na jioni, basi anza kumwgilia jioni tu, hii ni kwa sababu unaiandaa miche kuzoea hali ya shambani.

Wakati wa kupandikiza, ng'oa miche kwenye kitalu wakati kuna unyevu wa kutosha, au mwagilia maji kitalu chako kabla ya kung'oa miche. Using'oe miche kwenye kitalu wakati hakuna unyevu, utasababisha mizizi ya miche kukatika. Hali hii itapelekea miche kukauka mara tu baada ya kupandikiza.

Hakikisha unapandikiza miche yako wakati wa jioni, au wakati kuna mawingu, ukipandikiza wakati wa jua kali miche yako itakauka. Jambo lingine la muhimu hapa ni kwamba usichelewe kupandikiza miche yako baada ya 30 au 40, kwani itakua imekomaa sana na ikipandikizwa haitastawi. Jitahidi kupandikiza kabla ya siku 40, kuanzia siku ya 30 hadi 40 yenyewe.

Pia hakikisha shamba la kupandikiza miche lina unyevu wa kutosha, chimba mashimo ya kupandikiza miche yako yenye kina cha sm 3 na yenye nafasi ya sm 20 shina hadi shina na sm 60 - 75 mstari hadi mstari (sm 20 X sm 60 - 75).

Baada ya kuchimba mashimo hayo, weka mbolea ya samadi iliyooza vizuri kwa kiasi cha kiganja kimoja cha mkono wako kwa kila shimo kisha ichanganye vizuri mbolea hiyo na udongo.

Baada ya kuchanganya mbolea yako na udongo vizuri, panda miche yako mara tu baada ya kuing'oa kwenye kitalu, ili kupunguza atari ya kukauka. Fukia udongo vizuri kisha mwagilia maji, pia kwa wakati huohuo pawepo na mtu mwingine anayepulizia dawa ya kuvu na wadudu.

PALIZI
Kama ilivyo mazao mengine, zao la pilipili nalo huhitaji palizi kwa wakati. Nyasi zikizidi shambani mimea hudumaa na uzalishaji hupungua. Pia unaweza ukaweka matandazo ya nyasi kavu (mulching) shambani ili kuzuia upotevu wa maji hususani wakati wa kiangazi na kuzuia magugu kuota.



Makala na: Lusubilo A. Mwaijengo

Post a Comment

Previous Post Next Post