Kilomo bora cha Maparachichi - Sehemu ya kwanza (Growing Avocado - Part One)


KILIMO CHA MAPARACHICHI SEHEMU YA KWANZA

Parachichi (avocado)Persea americana ni tunda linolopendwa na kulimwa maeneo mengi ulimwenguni, tunda hili hutumika kama chakula, dawa au kutengenezea bidhaa mbalimbali. Tunda la parachichi lina mafuta yasiyo na madhara kwa afya ya binadamu (cholesterol free), hivyo tunda hilo husaidia kukinga mwili dhidi ya magonjwa ya moyo na baadhi ya magonjwa ya saratani. Vilevile tunda hili lina virutubusho mbalimbali kama vitamin B6, C, D na E. Tunda hili hutumika kwa matumizi mbalimbali kama; kuliwa jinsi lilivyo, kuchanganywa kwenye kachumbali, supu, pia hutumika kutengenezea mafuta (avocado oil), pafyumu n.k.

MAZINGIRA
Kulingana na aina ya parachichi, zao hili hufanya vizuri kwenye muinuko kuanzia m 0 - m 2100 kutoka usawa wa bahari. Pia parachi hupendelea joto kuanzia nyuzi joto 16ºC hadi 24ºC, joto la juu kabisa ambalo hufaa kwa zao hili ni nyuzijoto 33ºC, joto likizidi zaidi ya nyuzijoto 33ºC parachichi hodhoofu na kufa pia joto hilo likizidi na mionzi ya jua ya moja kwa moja matunda yaliyo wazi hupata muunguzo wa jua (sunburn). Vilevile kukiwa na baridi kali sana mpaka kukawa na ukungu basi zao la parachichi haliwezi kuota na kukua vyema.

Zao hili hufanya vizuri kwenye udongo wa aina mbalimbali ila inatakiwa uwe na kina cha kutosha, wenye uwezo wa kupitisha na kutunza maji pia wenye kiasi cha tindikali pH 5.5 – 6.5. Zao hili halipendi udongo unaotwamisha maji kwa sababu parachichi huathirika haraka sana kwenye udongo wenye maji mengi na tindikali nyingi.

Kiwango cha mvua kinachohitajika na kufaa kwa mwaka ni mm 1200, kiwango hiki kikipungua kisishuke zaidi ya mm 1000 kwa mwaka. Kama kutakua na uwepo wa maji ya kumwagilia, umwagiliaji usiwe zaidi ya mm 50 kwa mwagilio mmoja. Mazingira ya msimu wa masika na kiangazi hufaa sana kwa zao hili.

AINA
Kuna aina nyingi za maparachichi kulingana na maeneo husika, mara nyingi kuna maparachichi ya kienyeji na yale ya kisasa yaliyofanyiwa budding. Aina ya kienyeji huchukua muda mrefu kukomaa na kuanza kula matunda mpaka wastani wa miaka 6 hadi 10 kutegemeana na hali ya hewa, aina ya kisasa huchukua wastani wa miaka 3 hadi 5 kukomaa na kuanza kula matunda kutegemeana na hali ya hewa.

KUANDAA MICHE NA KUPANDA
Kabla ya kuandaa miche ni vyema kuchagua mbegu za parachichi zilizotoka kwenye mti bora unaotoa matunda mazuri na matamu. Chagua mbegu zenyeafya na zenye ukubwa kama wa yai alafu zipande kwenye maboksi au kwenye kitalu kabla ya kuziweka kwenye tyubu. Mara tu baada ya kuota ziamishe haraka sana mbegu hizo kwenye tyubu (polythene bags) au vyombo vyenye ukubwa wa lita 4. Zimwagilie mbegu hizo mpaka miche ifikie unene wa kalamu ya risasi (penseli).

Baada ya miche kufikia unene wa penseli ndio wakati wa kufanya budding (grafting), Budding ni kitendo cha kuunganisha mashina mawili ya mimea ya jamii moja kwa lengo la kuongeza ubora wa mti huo ikiwa ni pamoja na kuongeza uzalishaji na ubora wa matunda. 

Photo Credit: Gerald Holmes, Strawberry Center, Cal Poly San Luis Obispo, Bugwood.org licensed under a Creative Commons License ( CC BY-NC 3.0 US)

Kufahamu zaidi namna ya kufanya drafting tazama video ifuatayo;

Video Credit: Bang Jep Youtube channel

KUANDAA SHAMBA
Shamba kwa ajili ya kupanda miparachichi linapaswa liandaliwe vizuri na liwe safi, lisiwe na vichaka au visiki, shamba hilo linaweza kulimwa au likafyekwa.

KUPANDA
Baada ya kupanda shamba ni wakati wa kupandikiza miche kwa nafasi inayofaa kitaalamu, nafasi za kupanda maparachichi zipo nyingi kuanzia mita 6 - 9 kwa mita 7 - 10. Kabla ya kupanda chimba mashimo yenye ukubwa wa sm60 x sm60 x sm 60 yaani upana sm60, urefu sm60 na kimo kwenda chini sm60, kwa nafasi hii katika ekari moja huwa na miti 44 hadi 92.

Wakati wa kuchimba shimo tofautisha udongo wa chini na udongo wa juu alafu changanya udongo wa juu na samadi iliyooza vizuri kiasi cha ndoo kubwa moja ya lita 20 na kama utakua na mbolea ya minjingu (minjingu rock phosphate, ongeza kwenye mchanganyiko huo mbolea ya minjingu kiasi cha mkono mmoja au miwili kisha changanya vizuri.

Udongo wa chini uliobaki utandazwe kuzunguka mche mara tu baada ya kufukia mche, mara tu baada ya kupanda mwagilia maji ya kutosha kama ni msimu wa kiangazi. Kama ni msimu wa kiangazi weka matandazo ya majani makavu kuzunguka mche, majani hayo yanaweza yakawa ya ndizi au majani ya aina nyingine sharti yasiwe na miiba. Matandazo haya husaidia kuzuia upotevu wa maji hususani wakati wa kiangazi.

Kama umepanda miche yako kipindi cha masika hakuna haja ya kuweka matandazo labda kama maeneo yako yawe na mvua za wasiwasi zisizotabirika. Pia unaweza ukaiwekea kivuli miche yako mara tu baada ya kupanda kwa kutumia majani ya migomba au aina nyingine ya majani. Pia kama shamba lako lipo kwenye maeneo yenye upepo mkali, panda miti ya kuzuia upepo kuzunguka shamba lako. Upepo mkali husababisha mti kupukutisha majani, matunda na kusababisha michubuko ya matunda.

MATUMIZI YA MBOLEA
Zao la parachichi huweza kutoa mavuno kiasi cha Kilo 250 hadi 300 kwa mti mmoja kwa msimu mmoja, hii husababisha mahitaji makubwa sana ya virutubisho kwenye udongo. Kutambua kiasi gani cha virutubisho kinanachohitajika kuwenye kwenye udongo, inatakiwa udongo huo upimwe ili kubaini mapungufu. Kama kutakua changamoto kupima udongo unaweza ukatumia muongozo ufuatao ili kuongeza virutubisho kwenye udongo wa mti mmoja.


Makala na: Lusubilo A. Mwaijengo

Post a Comment

Previous Post Next Post