Yafahamu Makosa 13 ya kifedha yanayowafanya Watu wengi wasiimarike Kiuchumi

Habari ya majukumu ndugu wasomaji wangu?, Leo nimekuja na maada inayoelezea makosa mbalimbali ya kifedha tunayoyafanya kwenye maisha yetu ya kila siku. Watu wengi waliofanikiwa sana kiuchumi wanazungumzia jambo moja tu, nalo ni 'NIDHAMU YA FEDHA'. Jambo hili linameza ustaarabu wote wa matumizi ya fedha hata kama unapata kiasi kidogo tu kwa muda fulani. Kadiri unavyokua na nidhamu ya matumizi ya fedha ndivyo utakavyoona mabadiliko ya ukuaji wako wa uchumi kuongezeka. Yafuatayo ni baadhi ya makosa ya kifedha tunayofanya kila siku kwenye maisha yetu;

KOSA LA 1: KUANZA BIASHARA NA HELA YA MKOPO
Usikope pesa ya riba ili uanzishe biashara. Usitegemee pesa ya mkopo kuianzishia biashara, upate faida kisha uirudishe pesa ya mkopo na riba yake. 

KOSA LA 2: MATUMAINI YA PESA USIYOKUWA NAYO
Usitumie pesa ambayo bado haipo mikononi mwako. Wala usije ukamuahidi mtu kumpa pesa ambayo  umeahidiwa mahali fulani. Kama kuna mtu kakwambia, Flan njoo kesho nikulipe deni lako" Basi wewe usiende kukopa vitu kadhaa dukani au hata kumuahidi mtu mwingine kumpa pesa ambayo na wewe umeahidiwa.  Ni kosa. Unaweza kuingia kwenye matatizo.

KOSA LA 3: KULA FAIDA YA BIASHARA
Kama unataka kuhifadhi/kutunza pesa, kila unapopata pesa usianze kuitumia kwanza kisha ukategemea kutunza kiasi kitakachosalia. Hivyo basi,  ukipata tu pesa,  weka pembeni kiasi unachodhani kinafaa kutunzwa/kuhifadhiwa kisha tumia kiasi kilichobaki. 

KOSA LA 4: KUTOTAFUTA MAARIFA MAPYA YA BIASHARA
Ukipata nafasi ya kuonana na mtu tajiri, kamwe usiombe pesa.  Omba maarifa ya kutengeneza pesa kama yeye, tena kwa mtaji mdogo.  Maarifa ndio mtaji wa kwanza.  Unaweza kupewa/kusaidiwa pesa iwapo una mawazo mazuri ya kuzalisha pesa. Baadhi husema,  "Omba ndoano, usiombe samaki"

KOSA LA 5: KUHIFADHI PESA PASIPO KUIZALISHIA
Usitunze mbegu badala ya kuipanda.  Watu wengi hufurahia pesa wanayolipwa/kuipata  kisha wanaiweka bank au nyumbani bila kuiwekeza. Wekeza pesa ili uzalishe zaidi.  Usiogope kuingia hasara, kila aliefanikiwa alipoteza kwanza kabla hajafanikiwa. Wengi walipoteza muda, pesa, afya na hata matumaini ya kufanikiwa, ila kwa uthubutu wao, mwisho wa siku walifanikiwa.

KOSA LA 6: KUMKOPESHA MTU PESA AMBAYE UNAAMINI HATORUDISHA
Kamwe usimkopeshe mtu pesa ambayo unahisi hatorudisha.  Unapomkopesha mtu huyo pesa,  jiridhishe mwenyewe moyoni kuwa kama hatoweza kulipa basi deni lake halitoathiri urafiki wenu. Ukihisi kwamba kushindwa kwake kulipa kunaweza kuathiri urafiki wenu, basi mshauri aende bank akakope.

KOSA LA 7: KUMDHAMINI MTU AMBAYE HATOLIPA PESA ANAYODAIWA
Usikubali uwe shahidi , tena kwa kusaini kabisa ili umdhamini mtu ambae huna uhakika kuwa atalipa kile unachomdhamini. Kumbuka kuwa,  dhamana maana yake utawajibika iwapo atashindwa kulipa.

KOSA LA 8: KUTEMBEA NA PESA NYINGI ZISIZOKUA NA MATUMIZI
Epuka kutembea na pesa nyingi ambazo hata huna matumizi nazo wakati huo. Unaweza kujikuta unafanya matumizi ambayo hayakuwa kwenye ratiba sababu ya ushawishi wa pesa ya mfukoni. Ili kuepuka haya,  tembea na pesa uliyopanga kuitumia katika safari yako. Pesa nyingine itunze mahali pengine palipo salama. 

KOSA LA 9: KUTUNZA PESA MAENEO YASIYO SALAMA
Epuka kutunza pesa mahali pasipo sahihi.  Maeneo kama kwenye soksi,  sidiria,  chini ya mto wa kulalia,  chini ya begi,  kwenye kopo au hata kwenye begi la safari, si maeneo salama.  Ni rahisi kusahau,  kuibiwa au kupoteza pesa zako.  Ni bora ukatunza pesa kieletroniki; yaani bank au kwenye simu au kwenye pochi yenye kamba ngumu ya kuivaa mabegani au wallet ambayo inatosha kwenye mifuko imara na yenye vifungo kwenye nguo zako hasa uwapo safarini. 

KOSA LA 10: MATUMIZI YASIYOKUA YA LAZIMA
Usitumie pesa kwa kitu ambacho hakikuwa kwenye ratiba yako. Jiulize kwanza kabla hujanunua, "Bila kitu hiki, maisha yataenda au lah? Ukiona maisha yataenda bila kitu hicho, acha kukinunua. Tabasamu kisha ondoka.

KOSA LA 11: TAMAA YA KUNUNUA VITU MBALIMBALI
Usiingiwe tamaa kwa kununua kitu ambacho ungeweza kununua kwa bei ya punguzo mahali pengine zaidi. Labda tu uwe una pesa nyingi.

KOSA LA 12: MATUMIZI KUZIDI MAPATO
Matumizi yako ya pesa yasizidi pato lako. Unaweza kuwa una ndoto kubwa/matumizi makubwa ya pesa kuzidi pato lako.  Unapaswa kuwa bahili katika matumizi yako. Cheza na pato lako.  Fanya matumizi makubwa pale tu pato lako litakapoongezeka.  Hii itakuepushia kushindwa kufanya baadhi ya mambo ya msingi na kisha ukajikuta unaishia kwenye madeni makubwa. 

KOSA LA 13: KUKURUPUKA KUFANYA MAAMUZI
Una ndoto kubwa hapo baadae; labda kujenga nyumba,  kununua gari,  kununua kiwanja, simu nzuri hata pikipiki. Usikurupuke,  ukanunua kitu cha ndoto yako sasa eti tu sababu umekipata kwa bei ya punguzo. Usichanganye kati ya mahitaji ya baadae na ya sasa. Pesa unayotumia kutimizia ndoto sasa itumie kwa mahitaji ya sasa. Ndoto ibaki kuwa ndoto. Hii itakuepushia kuingia katika madeni au kuishi kwa shida sababu ya tamaa. Jipange taratibu kutimiza ndoto yako. 

Kama umependa au umeguswa na maada hii, mshirikishe mwenzako kwenye mitandao ya kijamii kwa kubofya hapo chini batani za Facebook, twitter, Whatsapp n.k.

Makala na: Lusubilo A. Mwaijengo

Post a Comment

أحدث أقدم