Kilimo bora cha Mihogo - Sehemu ya Sita (Growing Cassava - Part Six)


SEHEMU YA SITA

4. Cassava brown streak virus disease (Potyvirus - Potyviridae)
Ugonjwa huu husababishwa na virusi, huathiri sana maeneo ya pwani ya nchi ya Tanzania, Kenya, Msumbiji, Uganda na pwani ya chi ya Malawi mwambao wa ziwa Nyasa, pamoja na maeneo mengine kuzunguka jangwa la Sahara barani Afrika.

Namna unavyoenezwa
  • Ugonjwa huu huenezwa na mdudu anaeitwa 'whitefly' (Bemisia spp.). Wadudu hawa ni wadogo sana, wana mabawa na wana rangi nyeupe, hukaa na huzaliana chini ya majani. Kufahamu mdudu huyu rejea sehemu ya nne ya makala hii, kusoma makala hii BOFYA HAPA.
  • Pia ugonjwa huu huenezwa kupitia vipande vya mashina vya kupandia vilivyoathirika.

Athari
  • Majani huwa na rangi ya njano na mashina huwa na michilizi yenye rangi ya kahawia, pia mihogo huwa na michilizi yenye rangi ya kahawia.
  • Ugonjwa huu ni wa hatari sana kwa sababu majani yanaweza kuonekana yana afya nzuri wakati huo huo mihogo yote imekwishaoza chini ya udongo.

Namna ya kudhibiti
  • Tumia vipande vya mashina vya kupandia visivyo na ugonjwa.
  • Panda aina ya muhogo inayovumilia ugonjwa huu.
  • Ondoa mimea yote iliyoathirika shambani.

5. Anthracnose (Glomerella manihotis)
Huu ni ugonjwa unaosabishwa na fangasi aina ya Glomerella manihotis, huathiri majani na mashina.

 Photo Credit: Magdalena N. M. William, Ernest R. Mbega and Robert B. Mabagala © 2012, Cassava AnthracnoseDepartment of Crop Science and Production, Sokoine University of Agriculture, Morogoro, Tanzania

Athari
Majeraha au mabaka mabaka yenye umbo la mviringo huonekana kwenye mashina machanga. Kwenye mashina yaliyokomaa husababisha vijivimbe ambavyo baadae hubonyea, ugonjwa huu pia huathiri uzalishaji.

Namna ya kudhibiti

  • Panda aina ya mihogo inayovumilia ugonjwa huu (Resistance varieties)
  • Tumia vipande vya mashina vya kupandia vilivyo na afya nzuri na visivyokua na magonjwa
  • Hakikisha usafi wa shamba, ondoa na choma masalia yote ya majani na mashina yenye magonjwa baada ya kuvuna.

6. Magonjwa baada ya kuvuna (Post harvest diseases)
Haya ni magonjwa yanayoikumba mihogo baada ya kuvuna au pia baada ya kuikausha na kutengeneza makopa (Cassava chips), husababishwa na vimelea vya fangasi/Kuvu aina ya Rhizopus sp. na Aspergillus sp.

Athari
Husababisha mihogo kutengeneza fangasi na kuoza, hii hutokea endapo unyevu wa muhogo ukazidi asilimia 14%. Hali hii husababisha mihogo hiyo kutofaa kwa matumizi ya binadamu na wanyama.

Namna ya kudhibiti
  • Vuna mapema ili kuepusha au kupunguza mihogo kuoza ikiwa shambani.
  • Badirisha mazao kwa kupanda mazao mengine tofauti na muhogo kama mazao ya nafaka ikiwemo mahindi, ulezi, mtama n.k. hali hii itasaidia vimelea vya fangasi kutozoea shamba.

SHAMBA LA MIHOGO
Picha: Shamba la mihogo lililotunzwa vizuri


MAVUNO
Zao la muhogo huwa tayari kuvunwa baada ya miezi 9 hadi 12 tangu kupanda, pia inaweza kuvunwa mapema ikiwa itahitajika kwa chakula, mihogo ikichelewa kuvunwa huwa na nyuzi nyuzi. Aina ya muhogo inayokomaa mapema huwa tayari kuvunwa baada ya miezi 6 tangu kupanda, pia aina ya muhogo inayochelewa kukomaa huwa tayari kuvunwa baada ya miezi 12 tangu kupanda.

Mavuno hufanywa kwa kufukua mihogo kidogo kidogo au kuondosha mmea wote na kufukua mihogo yote. Mimea inayoelekea kukomaa huvunwa kidogo kidogo kwa ajili ya chakula kwa kufukua mihogo michache. Mihogo iliyokomaa hufukuliwa yote kuepusha mihogo kuwa na nyuzi nyuzi, endapo itakaa muda mrefu ardhini.

Picha: Kuvuna mihogo

Mihogo iliyovunwa hubakia na hali yake ya ubichi kwa siku 2 hadi 3, baada ya hapo hubadirika rangi ndani pamoja kuwa migumu ikipikwa. Mihogo yote haivunwi kwa siku moja, kwa hiyo inatakiwa mkulima avune kiasi kile tu ambacho kitatumiwa kwa siku hiyo au hadi kufikia siku tatu. Kama kuna uhitaji mkubwa wa soko hususani pale ambapo kutakua na wanunuzi wa uhakika watakaonunua shambani moja moja basi mkulima anaweza kuvuna mihogo yote kulingana na uhitaji wa mnunuzi. 

Wastani wa mavuno ya zao la muhogo ni kiasi cha Tani 3 - 4 za mihogo mibichi kwa ekari moja (3 - 4 Tonnes/acre) sawa na Tani 7.5 - 10 kwa hekta moja (7.5 - 10 Tonnes/Hectare). Endapo shamba litatunzwa vizuri kwa kufwata taratibu zote za kilimo bora huweza kutoa wastani mavuno kiasi cha Tani 10 kwa ekari moja (10 Tonnes/acre) sawa na Tani 25 kwa hekta moja (25 Tonnes/Hectare). Uwiano wa kiasi cha mihogo mibichi na mihogo mikavu iliyokatwa katwa na kuanikwa ni 3:1.


KUHIFADHI
Muhogo hautunziki vizuri ukiwa na ubichi wake, hivyo inatakiwa itolewe maganda, ikatwe vipande vipande na vianikwe juani. Inaweza kutunzwa kwa vipande vipande (Makopa) au Unga lakini sharti pawe na mazingira ya ukavu.

Picha: Kuandaa mihogo kwa ajili ya kuhifadhi

Picha: Mihogo iliyokaushwa (Makopa)


<<< SEHEMU YA TANO

*MWISHO WA MAKALA HII*

Kama una maoni au ushauri wowote kuhusiana na makala hii usisite kuacha maoni yako hapo chini, Karibu sana!

Makala na: Lusubilo A. Mwaijengo

Post a Comment

أحدث أقدم